Karatu: Mashine ya X-ray ya Kidigitali yazinduliwa Hospitali ya Karatu

Msaidizi wa Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Kaskazini Mch. Deogratius Msanya, amezindua mashine ya kidigitali ya uchunguzi kwa njia ya mionzi (Digital x-ray machine) katika hospitali ya Karatu Aprili 14, 2023.

Pamoja na uzinduzi wa mashine hiyo ya kisasa, pia Mch. Msanya aliweka wakfu mashine ya kufuatilia mwenendo wa mgonjwa (Digital patient monitor machine). Mashine zote mbili pamoja na gharama za kuzisimika zimegharimu kiasi cha shilingi milioni 137.

Aidha Mhe.  Msaidizi wa Askofu aliwashukuru marafiki kutoka Mission one word kutoka Ujerumani, marafiki toka jimbo la Aldof Bavaria na Jimbo la Bayreuth nchini Ujerumani ambao kwa pamoja walichangia kiasi cha shilingi milioni 116.

Akisoma risala kabla ya kuwekwa wakfu kwa machine hizo, Daktari kiongozi wa Hospitali ya Karatu Dkt. Heriel Zacharia alisema mashine zimegharimu kiasi cha shilingi milioni 116 zilizotolewa na wahisani toka Ujerumani na gharama ya kuzisimika milioni 21 zilizotolewa na Hospitali.

Hospitali ya Karatu inamilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dayosisi ya Kaskazini.